KLABU ya Simba imepigwa mweleka katika vita na mshambuliaji wake,
Ramadhan Singano ‘Messi’ kwenye mgogoro wao wa kimkataba uliodumu kwa
takribani miezi mitatu.
Maamuzi ya mgogoro huo yametolewa jana mbele ya waandishi wa habari
na Katibu Mkuu wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Selestine Mwesigwa
na kusema Simba imeshindwa kutekeleza masharti ya mkataba.
Alisema kuwa awali waliuagiza uongozi wa klabu hiyo wakayafanyie kazi
lakini hadi kikao cha jana kinakaa hakuna kilichotekelezwa.
“Awali TFF tulimwita Ramadhan Singano na uongozi wa Simba baada ya
kuwasikiliza kila mmoja tukaagiza wakae meza moja lakini Simba
hawakufanya hivyo na shauri hilo likalazimika kupelekwa kwenye Kamati ya
Maadili, Sheria na Hadhi za Wachezaji na Maamuzi yametoka kuwa mchezaji
Ramadhan Singano yupo huru kuanzia leo,” alisema Mwesigwa. Mwesigwa
alisema Kamati ya Sheria, Maadili na Hadhi za Wachezaji, iliwakilishwa
na Mwenyekiti Wakili Richard Sinamtwa na mchezaji Ramadhan Singano
alikuwa amefuatana na Mwenyekiti wa Sputanza, Mussa Kisoky na Katibu
Said George wakati Simba iliwakilishwa na Mwenyekiti wa Kamati ya
Usajili, Zacharia Hans Poppe na mjumbe wa Kamati ya Utendaji, Collin
Frisch na Mkurugenzi wa Wanachama wa TFF, Eliud Mvella. Kikao hicho
kilichukua karibu saa tano kumalizika huku kila upande ukilazimika
kutolewa nje wakati upande mwingine ukihojiwa mwishoni upande wa Simba
ulitoka ukiwa umenyong’onyea wakati Kisoky na wenzake wakitoka `meno’
nje huku wakikumbatiana na kuwadokeza waandishi: “Tumeshinda kijana yupo
huru ila sisi si wasemaji subirini TFF watatoa taarifa kamili.” Baadaye
gazeti hili lilimtafuta Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba,
Zacharia Hans Poppe na kuweka wazi kuwa hawajaridhishwa na maamuzi ya
kamati hiyo hivyo watakutana ili kujua hatua zaidi za kuchukua
ikiwezekana watakata rufaa kwenye Mahakama ya Usuluhishi ya Mambo ya
Michezo (CAS)ili kudai haki yao. “Tuliwasilisha ushahidi wote mbele ya
Kamati, tumeonesha mshahara wake ulikuwa kiasi gani na tumeonyesha kwa
nini alikuwa anapewa laki moja (100,000) zaidi. Lengo lilikuwa akalipie
kodi ya nyumba, lakini bado hatukueleweka. Tunaamini hapa si mwisho,
vipo vyombo vingine ambavyo vitatupa haki yetu, tunakwenda kukutana
kuangalia uwezekano wa kulipeleka suala hili huko.” Kamati ya Sinamtwa
imejiridhisha Messi hakuwahi kupewa nyumba ya kuishi na Simba jambo
ambalo ni kinyume cha mkataba baina yake na klabu hiyo, hivyo imemevunja
rasmi mkataba wake na kusema yupo huru kusajiliwa na klabu yoyote.
Messi alikuwa anailalamikia Simba kupeleka TFF mkataba wa miaka mitatu
wakati yeye alikuwa na mkataba wa miaka miwili na Simba, jambo
lililoleta utata hadi Sputanza kuamua kumsaidia na hatimaye Messi
kushinda. Messi alisajiliwa Simba miaka minne iliyopita kwenye Simba B
na baadae kuingizwa kwenye kikosi A baada ya uwezo wake kuwaridhisha
makocha mbalimbali ambao wamekuwa wakiifundisha Simba kwa nyakati
tofauti.
No comments:
Post a Comment