Friday, June 12, 2015

BAJETI MPYA HII HAPA



Kwa mara kwanza Bajeti ya 2015/16, ambayo ni ya mwisho ya Serikali ya Awamu ya Nne, haijaongeza kodi katika bidhaa za pombe na sigara, badala yake imeendelea kupandisha kodi katika mafuta huku ikiminya uingizaji wa bidhaa nchini kwa ajili ya kulinda viwanda na wazalishaji wa ndani na kuongeza ajira.
Pia, bajeti hiyo ya mwisho kwa utawala wa Rais Jakaya Kikwete imeweka kipaumbele katika kugharamia Uchaguzi Mkuu, kuweka msukumo maalum kwenye miradi ya umeme vijijini, maji vijijini, kukamilisha miradi ya kimkakati inayoendelea pamoja na kuwekeza kwenye rasilimali watu.
Bajeti hiyo imeeleza mikakati mbalimbali ya ukusanyaji mapato kwa kufanya mageuzi kwenye mfumo wa kodi, kudhibiti mianya ya matumizi ya fedha za Serikali, kupunguza misamaha ya kodi, kupunguza kero za wastaafu kwa kuwaongezea mafao ya mwezi kutoka Sh50,000 hadi Sh85,000, kupunguza Kodi ya Malipo ya Kadri ya Mapato (Paye) kwa asilimia moja na kuanzisha mafao ya kila mwezi kwa wazee.

Akiwasilisha bajeti hiyo ya mwaka wa fedha wa 2015/16, Waziri Mkuya alipendekeza mabadiliko ya sheria mbalimbali zitakazosaidia kupunguza na kuongeza kodi zitazoisadia Serikali kuongeza mapato ili iweze kufanikisha utekeleji wa bajeti ya Sh22.5 trilioni.
Waziri Mkuya aliliomba bunge liridhie mabadiliko katika Sheria ya Sheria ya Mafuta ya Petroli Sura namba 392 ili kuongeza tozo ya mafuta ya petroli na dizeli kutoka Sh50 hadi Sh100.
Pia, tozo ya mafuta ya taa imependekezwa kuongezwa kutoka Sh50 hadi Sh150 ikiwa ni moja ya njia ya kupunguza uwezekano wa uchakachuaji.
“Hatua ya kuongeza Tozo ya Mafuta ya Petroli inatarajiwa kuongeza mapato ya Serikali kwa kiasi cha Sh139.78 bilioni na fedha zote zitaelekezwa katika mfuko wa Rea kwa ajili ya utekelezaji wa mradi wa usambazaji umeme vijijini,” alisema Mkuya huku baadhi ya wabunge wakionyesha kupinga.
Pia, Mkuya alipendekeza mabadiliko katika Sheria Tozo za Mafuta na Barabara namba 220 ili kuongeza tozo katika mafuta ya Dizeli, Petroli na kwa Sh50 hadi kufikia Sh313.
Alisema hatua hiyo ya kuongeza tozo hiyo pia itaongeza mapato kwa takribani Sh136.4 bilioni ambayo alisema yataelekezwa katika mradi wa kusambaza umeme vijijini wa Rea.
Pamoja na maumivu hayo, Mkuya alipendekeza Waziri wa Fedha apatiwe mamlaka ya kusamehe Tozo ya Mafuta ya Petroli kwenye miradi inayotekelezwa kwa misaada ya wafadhili na yenye mikataba isiyohusisha utozaji wa tozo hiyo ili kuondoa usumbufu na ucheleweshaji katika utekelezaji wake.
Katika jitihada za kulinda viwanda vya ndani na kuongeza ajira, Serikali inapendeleza mabadiliko ya Sheria za Kodi ya Mapato namba 332, Sheria ya mauzo ya nje namba 196, Sheria ya Forodha ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya mwaka 2004 na Sheria ya Uwekezaji Tanzania Sura 196.
Waziri Mkuya alibainisha kuwa ili kumpunguzia mzigo mfanyakazi wamependekeza kupunguza kiwango cha chini cha kutoza kodi ya mapato ya ajira kutoka asilimia 12 hadi asilimia 11 akibainisha ni dhamira ya Serikali tangu mwaka mwaka 2006/07 kodi hiyo ilipokuwa asilimia 18.5.

No comments:

Post a Comment