Wednesday, December 11, 2013

ZITTO AWATOSA WAFUASI WAKE


Kigoma maandamanoMBUNGE wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe (CHADEMA), aliyevuliwa nyadhifa zote za uongozi kwa madai ya usaliti, amekemea vurugu zinazofanywa na baadhi ya wanachama wanaopinga uamuzi wa chama.
Zitto, amewataka wanachama wa CHADEMA kuwa watulivu na kuwaheshimu viongozi wa kitaifa wanaofanya kazi ya ujenzi wa chama mikoani.
Tangu Zitto avuliwe uongozi, baadhi ya wanachama wa CHADEMA wamekuwa wakifanya vurugu kwenye mikutano inayofanywa na Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dk. Willibrod Slaa, anayefanya ziara mkoani Kigoma.
Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, mwanasheria wa mbunge huyo, Albert Msando, alisema Zitto hahusiki na vurugu zinazoendelea katika ziara za Dk. Slaa.
Alisema Zitto anataka utulivu uwepo ndani ya chama kwakuwa anaamini sakata la kuvuliwa uongozi litamalizika bila kukiathiri chama.
“Zitto anasema amesikitishwa na matukio yanayotokea katika ziara ya Dk. Slaa ambayo sasa yamekuwa fujo zinazoendana na kurushiwa mawe, hahusiki na vurugu hizo,” alisema Msando kwa niaba ya Zitto.
Msando alisema licha ya vurugu hizo kuhusishwa na Zitto, kiongozi huyo ameweka wazi kuwa anaamini utulivu na heshima utakivusha chama katika kipindi hiki.
Zitto akata rufaa
Msando alisema Zitto amemuandikia barua Katibu Mkuu wa CHADEMA, kuelezea nia ya  kukata rufaa kwa Baraza Kuu la chama kupinga namna Kamati Kuu ilivyomvua nafasi za uongozi.
Alisema licha ya Zitto kufuata taratibu za chama kwa juzi kuwasilisha utetezi wake kutaka asivuliwe uanachama, pia ameamua kukata rufaa kupinga kuvuliwa vyeo alivyokuwanavyo.
Alizitaja sababu za kupinga uamuzi huo kuwa ni kukiukwa kwa utaratibu wa kuchukua hatua za kinidhamu.
Msando alisema kifungu cha kanuni ya Katiba ya CHADEMA  6:5:6 kinaeleza kuwa kiongozi yeyote hatachukuliwa hatua za kinidhamu bila kwanza kupewa mashitaka yake kwa maandishi na mamlaka husika na kupewa nafasi ya kujibu kwa maandishi.
Alisema kanuni ya uendeshaji 6.5.2 (a), (b), (c) na (d) kama ilivyorekebishwa Januari 2013 inasema: “Kwa mujibu wa ibara ya 5.4.3 na 5.4.4 ya katiba mwanachama yeyote hatachukuliwa hatua za kinidhamu ama kuonywa ama kuachishwa ama kufukuzwa uanachama bila kwanza; a) Kujulishwa makosa yake kwa maandishi na kutakiwa kutoa majibu katika muda usiopungua wiki mbili.
“b) Kupewa nafasi ya kujitetea mbele ya kikao kinachohusika, c) Mwanachama atajulishwa kwa maandishi uamuzi wa kikao mnamo wiki mbili baada ya kusikilizwa, d) Kamati Kuu inaweza kuchukua hatua za dharura bila kuzingatia utaratibu (b), (c) hapo juu kama itaona maslahi ya chama kwa ujumla yanaweza kuathiriwa isipokuwa mwanachama au kiongozi anayelalamikiwa atalazimika kuitwa kwenye kikao husika.”
Aliongeza kuwa Novemba 26  uongozi wa chama ulifanya mkutano na waandishi wa habari na kueleza kuwa marekebisho hayo ya kanuni ya mwaka 2013 ndiyo utaratibu uliofuatwa katika kuwavua uongozi Zitto na wenzake, na kwamba wakili Msando alidanganywa juu ya vifungu hivyo kwa kuwa vilishabadilishwa.
Alisema hatua ya dharura iliyochukuliwa na Kamati Kuu haikugusa kipengele (a) cha kanuni kinachoeleza kuwa kama Kamati Kuu itachukua hatua ya dharura kwa mujibu wa kipengele (d), bado kipengele (a) ni lazima kifuatwe na kwamba inatamka wazi sharti la kiongozi kupewa mashitaka kwa maandishi na kupewa nafasi ya kujibu kwa maandishi.
“Hii ni haki ya msingi kwa kila utawala au uongozi. Zitto Zuberi Kabwe hakupewa mashitaka yake aliyakuta ndani ya kikao baada ya kupewa taarifa kwa ujumbe wa simu (text message au sms),” alisema Msando.
Msando alisema kwa uzito wa makosa hayo yaliyosababisha kuvuliwa uongozi na kwa kuangalia athari zake kwa Zitto binafsi na chama kwa ujumla, Kamati Kuu ilitakiwa kujiridhisha kwamba kanuni za uendeshaji na katiba zinafuatwa.
Aliongeza kuwa utaratibu uliotumika kumvua Zitto na Dk. Kitila madaraka unaendana na utaratibu uliotumika kumvua uongozi Samson Mwigamba aliyekuwa kiongozi wa chama hicho Mkoa wa Arusha.
Alisema hadi sasa mteja wake hajapokea taarifa rasmi ya maandishi kwa mujibu wa kanuni za uendeshaji, zinazoonyesha kwamba ameshiriki kwenye kuandaa na kusambaza waraka unaosemekana ni mkakati wa ushindi wenye lengo la kupindua uongozi uliopo.
Msando aliongeza kuwa licha ya wahusaika wa waraka huo kusema kuwa Zitto hahusiki, Kamati Kuu iliamua kumuadhibu kwa hisia kutokana na urafiki wake na baadhi ya watuhumiwa.
Mwigamba aiburuza CHADEMA kwa msajili
Aliyekuwa Mwenyekiti wa CHADEMA Mkoa wa Arusha, Samson Mwigamba, aliyekuwepo kwenye mkutano huo, alisema amemuandikia barua Msajili wa Vyama vya Siasa nchini, Jaji Francis Mutungi, akimuomba atoe muongozo kuhusu mgogoro wa kikatiba uliopo ndani ya chama chao.
Alisema mwongozo huo unajikita kwenye kipengele kinachogusia ukomo wa uongozi kubadilishwa kinyume na utaratibu.
Mwigamba alisema Katiba ya CHADEMA ya mwaka 2004 kipengele 5.3.2 (c) kinasema kiongozi aliyemaliza muda wa uongozi ana haki ya kugombea na kuchaguliwa tena mradi awe anatimiza masharti ya kuchaguliwa kuwa kiongozi kwa muda usiozidi vipindi viwili katika cheo kimoja kwa ngazi moja.
Alibainisha kuwa Katiba ya CHADEMA ya mwaka 2006 kipengele cha 6.3.2 ( c) inayozungumzia muda wa uongozi kinasomeka kuwa kiongozi aliyemaliza muda wa uongozi ana haki ya kugombea na kuchaguliwa tena, mradi awe anatimiza masharti ya kuchaguliwa kuwa kiongozi, huku akibainisha kuwa sentensi kuhusu ukomo wa uongozi imeondolewa.
“Ni kweli kuwa marekebisho ya katiba yalifanyika mwaka 2006, lakini hoja ya pili ya kubadili kipengele hicho haikuwepo na muhtasari zinaonyesha wazi kuwa kulikuwa hakuna mjadala wa kipengele hicho au kuhusu suala zima la ukomo wa uongozi,” alisema Mwigamba.
Alisema si kweli kwamba CHADEMA haijawahi kuwa na katiba ambayo ina ukomo wa uongozi, na kwamba katiba ya  2006 haikuandikwa upya bali marekebisho yalifanywa kwa baadhi ya vipengele huku kipengele 5.3.2 (c ) kikiwa hakijawahi kujadiliwa.
Ziara ya Dk. Slaa
Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dk. Willibrod Slaa, jana aliendelea na ziara yake katika Jimbo la Kigoma Mjini ambako alisema hawatokubali viongozi na watendaji wa chama hicho wanaowekana mezani.
Dk. Slaa, alisema chama kimejiwekea utaratibu wa kuhakikisha kila kiongozi atapatikana kwa mujibu wa katiba ya chama hicho, akiwaagiza viongozi wa kanda 10 za chama hicho kuhakikisha wanasimamia suala hilo kama ilivyoagizwa kwenye waraka wa Katibu Mkuu namba 6.
Alisisitiza umuhimu wa chama hicho kufanya uchaguzi kuanzia ngazi ya chini ambayo ni msingi kwa kila kitongoji au mtaa, huku kikijiandaa kuwa na mabalozi wa nyumba 10.
Aidha, Dk, Slaa alisema kuwa suala la makada waliovuliwa nafasi zao za uongozi halijafika mwisho.
“Suala la Zitto na wenzake wawili wala sitalizungumzia kwa sababu taratibu za chama kupitia vikao hazijakamilika. Lakini nitazungumzia maneno ya upotoshwaji yanayoendelea kuhusu suala hili, yako kwenye mitandao, yako vijiweni na wengine hawajui wanayapokea tu na kufikiri ndiyo ukweli,” alisema.

No comments:

Post a Comment