Saturday, August 22, 2015

LOWASA MAGUFULI WAPETA MTIKILA STOP

 

Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) imewapitisha wagombea wa vyama vinane  kugombea nafasi ya urais na umakamu jana jijini Dar es Salaam huku vyama vitatu vikiondolewa kushiriki katika kinyang’anyiro hicho.
 
Vyama vilivyoondolewa ni cha Democratic Party (DP) kilichomsimamisha mgombea urais  Mchungaji  Christopher Mtikila, Chama Cha Kijamii (CCK)  na ADA –Tadea, kwa kutotimiza vigezo vinavyotakiwa na Nec.
 
Fomu hizo zilitolewa kwa wagombea 12 lakini hadi  jana vyama 11 vilirejesha wakati chama cha AFP kikiingia mtini.
 
Chama cha kwanza kurejesha fomu kilikuwa ni Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), mgombea wake anayeungwa na vyama vinaungwa na Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), Edward Lowassa  alingia katika ofisi hizo  saa 3:40 asubuhi akiwa na msafara wa magari saba.
 
Wa kwanza kufika katika ofisi hizo alikuwa Katibu Mkuu wa Cuf, Maalim Self  baada ya magari mawili kupita ndipo gari la Lowassa lilifuatia akiwa na Mgombea mwenza, Juma Haji Duni.
 
Hata hivyo, wapambe wengine alioongoza nao akiwemo Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia waliingia kiaina huku  kila mmoja akifika kwa muda wake na kumfuata mheshimiwa Lowassa aliyekuwa ndani ya ofisi za Nec.
 
Baada ya fomu kupitishwa na Nec, Lowassa aliwaambia Waandishi wa habari kuwa amemaliza kazi salama na tayari wamepata wadhamini pande zote mbili (Bara na Zanzibar).
 
Saa 5:00 Chama cha Mapinduzi kikiongozwa na Mgombea urais wake, Dk. John Magufuli, alifuatana na Makamu wake Samia Hassan Suluhu katika ofisi za Nec wakiwa na msafara wa magari manne.
 
Dk. Magufuli alisema sasa wameanza kazi rasmi kwa kuwa wametimiza masharti yote waliyotakiwa. 
 
Alisema kampeni zitazinduliwa kesho na mengi yataelezwa wakati wa uzinduzi “naomba mniombee kwa Mungu ili nimalize safari yangu.”
 
Vyama vingine vilivyofuatia ni Tanzania Labour Party (TLP),  kikiwa na mgombea wake wa urais, Machmillan Lyimo, akiwa na mgombea mweza Hussein Juma Salim, Alliance for Democratic Change ( ADC), mgombea urais Chief Lutalosa Yemba ,akiwa na mgombea mweza Said Abdallah.
 
Vingine ni Chama ACT-Wazalendo kilichowasilishwa na mgombea, Anna Mghwira akiwa na mgombea mweza Hamad Yusuf, Chama cha N.R.A  Mgombea Urais ni Janken Kasambala akiwa na mgombea mweza Simai Abdulla na chama cha Chauma kikiwakilishwa na Hashim Rungwe akiwa na mwenza wake Issa Hussein.
 
Alisema ajira ndio kipaumbele chake akidai yeye ndiyo mwenye uzoefu katika siasa kuliko wengine.
 
Wakati zoezi hilo likiendelea, baadhi walisahau vitu muhimu akiwemo Rungwe ambaye alifika katika ofisi hizo akiwa hana picha hali ambayo ilimlazimu kuzifuata.
 
Wagombea hao walipitiwa  baada ya Mkurugenzi wa Tume ya Uchaguzi (NEC), Kailima Kombwey, kuthibitisha wamekidhi vigezo vyote vinavyotakiwa na kumuomba Mwenyekiti wa NEC, Jaji Damian Lubuva kutangaza majina kwa uthibitisho.
 
Alivitaja vigezo viliyokuwa vikiangaliwa ni pamoja na tamko la mgombea kujazwa, tamko la kisheria kujazwa, majina ya wadhamini 200 kwa kila mkoa kujazwa kikamilifu,udhibitisho wa chama, mgombea kuweka dhamana ya sh milioni 1 
 
Mwenyekiti wa Nec Jaji Lubuva alisema wagombea hao wanane wamepitishwa rasmi kuanza kufanya kampeni za ugombea urais.
 
Wagombea waliopita wamepatiwa nyaraka sita ikiwemo Katiba ya Jamhuri ya Muungano ya mwaka 1977

No comments:

Post a Comment