Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) imewapitisha wagombea wa vyama vinane
kugombea nafasi ya urais na umakamu jana jijini Dar es Salaam huku
vyama vitatu vikiondolewa kushiriki katika kinyang’anyiro hicho.
Vyama vilivyoondolewa ni cha Democratic Party (DP)
kilichomsimamisha mgombea urais Mchungaji Christopher Mtikila, Chama
Cha Kijamii (CCK) na ADA –Tadea, kwa kutotimiza vigezo vinavyotakiwa na
Nec.
Fomu hizo zilitolewa kwa wagombea 12 lakini hadi jana vyama 11 vilirejesha wakati chama cha AFP kikiingia mtini.
Chama cha kwanza kurejesha fomu kilikuwa ni Chama cha Demokrasia na
Maendeleo (Chadema), mgombea wake anayeungwa na vyama vinaungwa na
Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), Edward Lowassa alingia katika
ofisi hizo saa 3:40 asubuhi akiwa na msafara wa magari saba.
Wa kwanza kufika katika ofisi hizo alikuwa Katibu Mkuu wa Cuf,
Maalim Self baada ya magari mawili kupita ndipo gari la Lowassa
lilifuatia akiwa na Mgombea mwenza, Juma Haji Duni.
Hata hivyo, wapambe wengine alioongoza nao akiwemo Mwenyekiti wa
Chadema, Freeman Mbowe na Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia
waliingia kiaina huku kila mmoja akifika kwa muda wake na kumfuata
mheshimiwa Lowassa aliyekuwa ndani ya ofisi za Nec.
Baada ya fomu kupitishwa na Nec, Lowassa aliwaambia Waandishi wa
habari kuwa amemaliza kazi salama na tayari wamepata wadhamini pande
zote mbili (Bara na Zanzibar).
Saa 5:00 Chama cha Mapinduzi kikiongozwa na Mgombea urais wake, Dk.
John Magufuli, alifuatana na Makamu wake Samia Hassan Suluhu katika
ofisi za Nec wakiwa na msafara wa magari manne.
Dk. Magufuli alisema sasa wameanza kazi rasmi kwa kuwa wametimiza masharti yote waliyotakiwa.
Alisema kampeni zitazinduliwa kesho na mengi yataelezwa wakati wa
uzinduzi “naomba mniombee kwa Mungu ili nimalize safari yangu.”
Vyama vingine vilivyofuatia ni Tanzania Labour Party (TLP), kikiwa
na mgombea wake wa urais, Machmillan Lyimo, akiwa na mgombea mweza
Hussein Juma Salim, Alliance for Democratic Change ( ADC), mgombea urais
Chief Lutalosa Yemba ,akiwa na mgombea mweza Said Abdallah.
Vingine ni Chama ACT-Wazalendo kilichowasilishwa na mgombea, Anna
Mghwira akiwa na mgombea mweza Hamad Yusuf, Chama cha N.R.A Mgombea
Urais ni Janken Kasambala akiwa na mgombea mweza Simai Abdulla na chama
cha Chauma kikiwakilishwa na Hashim Rungwe akiwa na mwenza wake Issa
Hussein.
Alisema ajira ndio kipaumbele chake akidai yeye ndiyo mwenye uzoefu katika siasa kuliko wengine.
Wakati zoezi hilo likiendelea, baadhi walisahau vitu muhimu akiwemo
Rungwe ambaye alifika katika ofisi hizo akiwa hana picha hali ambayo
ilimlazimu kuzifuata.
Wagombea hao walipitiwa baada ya Mkurugenzi wa Tume ya Uchaguzi
(NEC), Kailima Kombwey, kuthibitisha wamekidhi vigezo vyote
vinavyotakiwa na kumuomba Mwenyekiti wa NEC, Jaji Damian Lubuva
kutangaza majina kwa uthibitisho.
Alivitaja vigezo viliyokuwa vikiangaliwa ni pamoja na tamko la
mgombea kujazwa, tamko la kisheria kujazwa, majina ya wadhamini 200 kwa
kila mkoa kujazwa kikamilifu,udhibitisho wa chama, mgombea kuweka
dhamana ya sh milioni 1
Mwenyekiti wa Nec Jaji Lubuva alisema wagombea hao wanane wamepitishwa rasmi kuanza kufanya kampeni za ugombea urais.
Wagombea waliopita wamepatiwa nyaraka sita ikiwemo Katiba ya Jamhuri ya Muungano ya mwaka 1977
No comments:
Post a Comment