Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahim Lipumba
amechukua fomu ya kugombea urais kupitia chama hicho na kuahidi
kupambana na rushwa huku akishangaa kuwapo watuhumiwa wa ufisadi
waliotakiwa kuwa mahabusu lakini wakichukua fomu za kuwania nafasi hiyo
kupitia CCM.
Profesa Lipumba alisema iwapo atapatiwa ridhaa na
Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), kupeperusha bendera ya umoja huo
atahakikisha anaunda Katiba yenye maoni ya wananchi na Serikali ya Umoja
wa Kitaifa ili kuwaunganisha Watanzania dhidi ya ufisadi.
Mwanasiasa huyo mkongwe katika upinzani aliwaambia
wafuasi wa CUF waliomsindikiza kuchukua fomu hiyo jijini hapa jana kuwa
ameamua kuwania kiti hicho kwa mara ya tano kwa kuwa kati ya viongozi
wa juu wa Ukawa anaamini ana sifa, uwezo, uadilifu, uwazi, uwajibikaji
wa kuwaunganisha Watanzania ili waondokane na rushwa na ufisadi
uliokithiri nchini.
Profesa Lipumba aliyekabidhiwa fomu hiyo na Katibu
wa CUF Wilaya ya Kinondoni, Mohamed Mkandu saa 6.55 mchana, alitaja
vipaumbele vyake kuwa ni kujenga misingi ya kuhakikisha watoto wanapata
fursa sawa ya maendeleo, ajira, afya, kulinda rasilimali za umma na
kupambana na ufisadi.
Profesa Lipumba aliyeanza hotuba yake ya takriban
dakika 45 kwa kutoa wasifu wa usomi na kazi mbalimbali za kiuchumi
alizozifanya kwa takriban miaka 40, alisema anafahamu bayana matatizo
mengi ya Watanzania kwa kuwa amezaliwa na kukulia kijijini.
Alisema matatizo hayo yamesababishwa na “siasa
mbovu za chama cha mapinduzi” ukiwamo ufisadi, hivyo iwapo atapatiwa
ridhaa ya kuwania kiti hicho cha juu, atakuwa na kazi kubwa ya kuleta
uongozi makini utakaohakikisha rasilimali za nchi zinatumika kwa
maendeleo ya watu wote.
Alisema iwapo atachaguliwa kuwa rais, hatakuwa na
msalie mtume na mafisadi na wote wanaohusika watawajibika kwa mujibu wa
sheria na taratibu.
“Inatisha sana kuona mafisadi wakubwa, wala rushwa
wakubwa badala ya kuwa ndani ya jela, wanachukua fomu za urais.
Tunahitaji kwa kufuata taratibu na haki, mafisadi hao watumikie vifungo
na mali zilirudishwe kwa umma walikofisadi,” alisema Profesa Lipumba
huku akishangiliwa na wafuasi wa chama hicho.
Iwapo atapatiwa nafasi ya urais, alisema katika
utawala wake atahakikisha watoto nchini wanapatiwa fursa sawa ya
maendeleo kwa kutoa huduma bora afya, lishe na elimu.
Alisema suala la ukuaji imara kwa watoto
halijapatiwa kipaumbele na kusababisha udumavu unaowanyima uwezo mkubwa
wa kufikiri pindi wanapokuwa wakubwa.
Kufumua Katiba inayopendezwa
Mwanasiasa huyo alisema anachukua fomu nchi ikiwa
njia panda baada ya Katiba Inayopendekezwa kuacha masuala ya msingi ya
uadilifu na uwajibikaji na kusababisha wachache kujinufaisha kwa rushwa.

No comments:
Post a Comment