MWENYEKITI wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Freeman
Mbowe, amesema kuwa chama chake hakiwezi kuvumilia usaliti wa aina
yoyote unaofanywa na makada na viongozi wasio waaminifu.
Sambamba na hilo, mwenyekiti huyo ametamba kuwa kamwe hawezi
kununulika kwani hana njaa na hata Chama Cha Mapinduzi (CCM) kinajua
hivyo.
Mbowe alisema: “Bahati mbaya Mbowe sinunuliki, hela sina na sina
njaa, lakini sinunuliki na nzuri zaidi katibu mkuu wetu Dk. Slaa naye
hanunuliki na CCM wanalijua hili.”
Akizungumza kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika katika viwanja vya
Malimbe mjini hapa, ikiwa ni siku ya kwanza ya ziara yake mkoani Mwanza,
Mbowe alisema CHADEMA hakitawafumbia macho viongozi au wanachama wasio
waaminifu.
Ingawa Mbowe hakumtaja mtu kwa jina, lakini hotuba yake ilionyesha
dhahiri kumlenga Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe, aliyekuwa
Mwenyekiti wa CHADEMA Mkoa wa Arusha, Samson Mwigamba na Mjumbe wa
Kamati Kuu aliyevuliwa uongozi, Dk. Kitila Mkumbo.
Viongozi hao hivi karibuni walivuliwa nafasi zao za uongozi na kupewa
siku 14 za kujieleza kwanini wasifukuzwe uanachama kwa madai ya
kukisaliti chama.
“Tumejenga chama makini kwa gharama kubwa sana na sasa kimekuwa
tumaini la Watanzania, kwa hiyo hatuwezi kumvumilia mtu au watu kwa
kufumbia macho wanapokwenda kinyume na misingi ya chama.
“Yaani mpo safarini ndani ya bahari au ziwa, halafu mnafika katikati
ya bahari mtu au watu wanaanza kutoboa boti yetu, hivi huyo mtu
utamwacha hivi hivi? Mkimuacha lazima mzame wote, hivyo lazima azame
yeye,” alisema Mbowe.
Mwenyekiti huyo ambaye pia ni Mbunge wa Hai, alisema CHADEMA
haitishwi wala kubabaishwa na propaganda na njia pandikizi zinazofanywa
kwa kuandamana na mabango kupinga uamuzi wa Kamati Kuu ya CHADEMA wa
hivi karibuni ambao viongozi wanaodaiwa kukisaliti chama waliadhibiwa.
Alisema kuwa hata yeye pamoja na Katibu Mkuu wake, Dk. Willibrod Slaa
wako tayari kuvuliwa nyadhifa zao na hata kufukuzwa uanachama
wakibainika wanakihujumu chama.
Kiongozi huyo wa kambi rasmi ya upinzani bungeni, alisema kuongoza
chama kikuu cha upinzani kama CHADEMA ni kazi kubwa na hakuna
majaraibio.
Aliwaomba wanachama makini wajitokeze kugombea nafasi yoyote pale uchaguzi utakapoitishwa.

No comments:
Post a Comment