Wednesday, April 17, 2013

JESHI LA POLISI KATIKA KASHIFA NZITO

JESHI la Polisi Mkoa wa Temeke jijini Dar es Salaam limeingia katika kashfa ya kuwalazimisha ndugu wa mtuhumiwa aliyefia mikononi mwao watoe fedha za kununulia mafuta ya sh 40,000 kwa ajili ya kusafirisha mwili wa marehemu kwenda kuufanyia uchunguzi.

Tanzania Daima lilidokezwa jana kuwa ndugu hao walifika Kituo cha Polisi Temeke juzi kwa ajili ya kuomba mwili wa marehemu ufanyiwe uchunguzi kufuatia kifo chake kutawaliwa na utata, huku watuhumiwa wa mauaji hayo nao wakiwa bado hawajakamatwa.

Katika sakata hilo, ndugu wa marehemu Gasper Augustino Mlay, wanalituhumu jeshi hilo Mkoa wa Temeke kwa kumpiga na kumsababishia kifo mpangaji huyo aliyeshindwa kuhama kwa muda aliopangiwa na mwenye nyumba wake, Aprili 13, mwaka huu.
Wakizungumza na gazeti hili, ndugu wa marehemu, Peter Masoy na Elizabeth Mlay, walisema kuwa Gasper alikuwa amepewa notisi ya kuhama ndani ya siku 30 lakini hakuweza kufanya hivyo kwani hadi siku ya tukio alikuwa bado anasubiri kupata fedha.
Waliongeza kuwa siku hiyo mwenye nyumba alifika kumhamisha ndugu yao akimwamuru atoke, yapata saa 12 asubuhi, lakini alikataa, akaomba kupambazuke, hivyo akajifungia ndani.
“Kitendo hicho kilimfanya mwenye nyumba kumwita mjumbe wa mtaa huo, wakaenda polisi, wakarejea katika nyumba hiyo wakavunja mlango na kumpiga hadi alipozidiwa ndipo wakamchukua kumpeleka Kituo Kidogo cha Polisi Sandali.
“Lakini wakiwa njiani Gasper aliwaomba awapatie namba za simu ili waweze kutuita ndugu kwa ajili kumdhamini. Mwenye nyumba na askari huyo walikubali kutupigia na tukafika,” walisema.
Waliongeza kuwa mdogo wa marehemu Elias Mlay alipelekwa hadi alipokuwa akipanga kaka yake ili kukagua uharibifu uliosababishwa na ndugu yao.
“Kwa kuwa uharibifu haukuwa mkubwa, hivyo aliomba kulipa sh 20,000 kwa askari Moses Zimba ili wayamalize badala ya sh 300,000.
“Lakini tulipokwenda kituoni ili kumwona ndugu yetu na kumdhamini, tulikuta amefariki dunia huku akiwa na uvimbe mkubwa tumboni. Tulipeleka taarifa Kituo cha Polisi Chang’ombe ambao walitoa gari na kuja kuchukua mwili wa marehemu kuupeleka Hospitali ya Temeke,” walisema.
Ndugu hao waliongeza kuwa polisi waliwaambia kwamba walikuwa wamechelewa hivyo kuwataka warudi jana kwa ajili ya kuufanyia uchunguzi mwili huo.
“Tulipofika kituoni tuliambiwa kuwa uchunguzi huo hautafanyika hapa Hospitali ya Temeke bali Hospitali ya Taifa Muhimbili lakini kwanza tukatakiwa tulipe sh 40,000 kwa ajili ya mafuta ya gari,” walisema.
Walifafanua kuwa walielezwa kwamba Hospitali ya Temeke hairuhusiwi kufanya uchunguzi wa mwili wa ndugu yao kwa kuwa ulikuwa na utata sana.
 Kutokana na mkanganyiko huo, gazeti hili lilimtafuta Mganga Mkuu wa Hospitali ya Temeke, ambaye naye alielekeza Katibu Tawala wa hospitali hiyo aweze kufafanua kuhusu suala la uchunguzi wa mwili.
Katibu huyo alisema Hospitali ya Temeke ni ya mkoa hivyo hutoa huduma za uchunguzi, hivyo mwili wa marehemu Gasper haukuwa na sababu ya kupelekwa Muhimbili.
Alipotafutwa kufafanua juu ya sakata hilo, Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Temeke, Englibert Kiondo, alikiri kuwa magari ya polisi hayakuwa na mafuta, lakini akasema si kitendo kizuri kwa askari kuomba mafuta kutoka kwa ndugu wa marehemu.
Kamanda Kiondo aliagiza mwili huo uchunguzwe huku akiwahakikishia ndugu wa marehemu kuwa watuhumiwa wa mauaji hayo, yaani mwenye nyumba pamoja na mtu aliyetambulishwa kama polisi shirikishi tayari wanashikiliwa na polisi.  
Hata hivyo, taarifa zaidi zimesema kuwa ndugu wa marehemu walikuwa wakishinikizwa na polisi kuuchukua mwili huo kwa kisingizio kuwa marehemu alifariki dunia kwa kudhuriwa na moshi uliotokana na nyumba kuwaka.
Alipotafutwa kwa simu mtuhumiwa wa mauaji hayo anayetajwa kuwa ni askari, alikiri kupatwa na tatizo hilo lakini akamuomba mwandishi waonane ana kwa ana wayamalize kabla ya kukamatwa.
Katika hatua iliyoonesha kuwapo kwa  mkanganyiko mkubwa, Kamanda Kiondo aliwasiliana na mwandishi wa gazeti hili na kumwita ofisini kwake, lakini alipofika alimwelekeza akaonane na Mkuu wa Upelelezi ili asome faili na kuangalia fomu ya uchunguzi.
Alitamba kuwa uchunguzi wa mwili wa marehemu ulikuwa umefanyika, jambo ambalo halikuwa la kweli.
Gazeti hili kama lilivyoelekezwa na Kiondo lilifika ofisini kwa Mkuu wa Upelelezi ambaye naye aliomba asubiriwe kwani alikuwa na wageni.
Wakati mwandishi akisubiri nje, alipigiwa simu na Kamanda Kiondo lakini kwa kutumia simu tofauti akimuuliza: “Hivi wewe ndiye umesema unatoka CHADEMA?” Alipojitambulisha kuwa ni mwandishi wa habari, Kamanda Kiondo akakata simu.
Baadaye kamanda huyo alimpigia simu mwandishi na ndugu wa marehemu pamoja na aliyekuwa askari aliyekuwa akipeleleza tukio hilo ili akutane nao ofisini.
Hata hivyo baada ya ndugu wa marehemu kusema tayari wameleta fedha waliyoombwa kwa ajili ya mafuta, polisi waligeuka wakidai: “Mlisikia vibaya, sisi mafuta tumeshaleta, ni mara nyingi tunajitolea fedha zetu za mfukoni kuweka mafuta kwenye magari.”

No comments:

Post a Comment