Monday, February 11, 2013

MWANAFUNZI AWAWA KWAKUCHINJWA NA KISU

MWANAFUNZI wa darasa la sita katika Shule ya Msingi ya Kasumulu, kata ya Ngana, wilayani Kyela, Kaselema Mpale (14), ameuawa kikatili kwa kuchinjwa na kisha kunyofolewa baadhi ya viungo sehemu ya mwili wake.

Akizungumza na Tanzania Daima juzi, mama wa mtoto huyo, Lucia Kamnyonge, alisema kuwa tukio hilo lilitokea Ijumaa saa 10:30 akiwa ametumwa na baba yake kwenda nyumba ya jirani kuchukua mpunga ambao ungetumika kama chakula cha siku hiyo.

Alisema kuwa toka siku hiyo hakupatikana hadi alipokutwa kesho yake akiwa amekufa kwa kuchinjwa na kisu na kunyofolewa baadhi ya sehemu zake za mwili kama pua, mdomo, jicho, sehemu zake za siri na kuchunwa ngozi ya kichwa karibu na utosi na mwili wake kutundikwa juu ya mti.
Alisema kuwa baada ya kutoonekana, taarifa ilipelekwa kwenye ofisi ya serikali ya kijiji ambapo uliitishwa mkutano wa wananchi wote wa kijiji hicho na kuanza kumtafuta mtoto huyo bila ya mafanikio.

Baadaye baba yake alikuta mwili wake juu ya mti ukiwa umetundikwa kichwa chini miguu juu na viungo vyake hivyo vikiwa vimenyofolewa.

Mwenyekiti wa kitongoji cha Ibungumbati, kijiji cha Ushirika, Adamu Mkese, alisema kuwa tukio hilo limewashtua wananchi wa eneo hilo na kwamba katika mkutano wa dharura wa kijiji, wananchi walimhusisha baba wa mtoto huyo, Mpale Mbisa (35), katika mauaji hayo.

Alisema kuwa wanakijiji walitilia shaka kutokana na mazingira ya kifo chenyewe na maelezo ya kujichanganya aliyoyatoa baba huyo hasa jinsi alivyomkuta mtoto huyo akiwa amekufa katika eneo ambalo wananchi walipita usiku na mchana wakimtafuta bila kumuona.

Wananchi walimtuhumu baba huyo kuwa alichukua fedha sh milioni saba ili kumuuza mtoto wake. Tuhuma hizo zilililazimu Jeshi la Polisi kumkamata mzazi kwa ajili ya mahojiano zaidi.

Naye ofisa mtendaji wa kijiji hicho, Naomi Charles, alisema kuna dalili zote za baba huyo kuhusika katika mauaji hayo kutokana na mazingira.

Alisema hisia hizo za wananchi zinaweza kuwa na ukweli ndani yake na kuwa Jeshi la Polisi inabidi lifanye uchunguzi wa kina na kuwa kama ataachiwa usalama wake utakua mdogo pale kijijini.

Ofisa tarafa ya Unyakyusa, Lwitiko Mwakalukwa, alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kwamba yeye pamoja na mkuu wa wilaya walifika eneo la tukio na kujionea unyama huo.

No comments:

Post a Comment