Saturday, February 9, 2013

JERA KWAINGILIA MSAFARA WA WAZIRI

 
DEREVA maarufu wa pikipiki za abiria ‘bodaboda’ mjini Mpanda, Selemani (35) amehukumiwa kifungo cha miezi mitatu jela kwa kosa la kuingilia msafara wa Waziri Mkuu Mizengo Pinda wakati wa ziara yake mkoani Katavi hivi karibuni.

Hukumu hiyo ilitolewa juzi na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Mpanda, Chiganga Tengwa, na kuwashitua wakazi wengi wa mjini Mpanda.


Awali Mwendesha Mashitaka wa Polisi, Ally Mbwijo aliiambia mahakama kuwa Selemani, maarufu kwa jina la Baunsa alitenda kosa hilo Desemba 16 mwaka jana majira ya saa 11 jioni katika eneo la benki ya CRDB wakati Pinda alipokuwa akirejea nyumbani kwake Mtaa wa Makanyagio akitokea wilayani Mlele.

Alieleza mahakamani hapo kuwa, pamoja na Selemani kusimamishwa na askari wa usalama barabarani ili aupishe kwanza msafara huo, hakuweza kutii agizo hilo, jambo ambalo lilikuwa ni hatari.

Aliongeza kuwa, polisi waliamua kumfukuza na kumkamata, lakini aliwagomea kumpeleka kituo cha polisi kwa kile alichodai hawezi kwenda hadi atakapofika Kamanda wa Polisi wa Mkoa kwa kile alichokidai askari wa usalama barabarani wamemuonea.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Katavi, Dhahiri Kidavashari ambae nae alikuwa kwenye msafara huo, alifika kwenye eneo hilo na kuamuru mwendesha pikipiki huyo apelekwe kituo cha polisi, agizo ambalo lilitekelezwa na mshitakiwa alitii amri.


Makosa mengine yaliyokuwa yakimkabili mshtakiwa huyo ni pamoja na kuendesha pikipiki akiwa amelewa, kuendesha pikipiki bila leseni na kukaidi amri halali ya polisi.

Hakimu Tengwa baada ya kusikiliza kesi hiyo alisema mahakama imeridhika na ushahidi na utetezi na kumtia hatiani, akamhukumu kulipa sh laki tano ama kwenda jela miezi mitatu, licha ya mshitakiwa kuomba aachiwe huru akidai askari waliomkamata kwenye eneo hilo walimfananisha.

No comments:

Post a Comment