Thursday, November 15, 2012

FAMILIA ZA WASHITAKIWA WA VURUGU ZANZIBAR WAMUANDIKI BARUA WAZIRI

FAMILIA za washtakiwa wanane katika kesi za uchochezi Zanzibar wameandika barua kwa Waziri wa Katiba na Sheria na taasisi zingine, wakilalamikia ukiukwaji haki za binadamu.
Pia, barua hiyo imepelekwa kwa Mkurugenzi wa Kituo cha Sheria Zanzibar, Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu cha Tanzania kilichopo Dar es Salaam, Amnesty International na ofisi za balozi za nje nchini.
Katika barua hiyo ya Novemba 13, mwaka huu familia zinazolalamika ni za Sheikh Farid Hadi Ahmed, Msellem Ali Msellem, Azzan Khalid Hamdan, Mussa Juma Issa, Suleiman Juma, Khamis Ali, Hassan Bakari na Gharib Ahmad ambao wanakabiliwa na kesi mbili za uchochezi Mahakama Kuu Zanzibar na Mwanakwerekwe.
Barua hiyo ambayo imetiwa saini na watu wanane wa familia hizo, wanadai  ndugu zao wanachukuliwa zaidi ya wafungwa wakati ni mahabusu na wanatuhumiwa tu na mahakama haijawatia hatiani.
Mambo ambayo wanadai kuwa wanafanyiwa, ni kuzuiwa kubadili nguo kwa muda wa zaidi ya wiki tatu na hawaruhusiwi kuletewa zingine kutoka nyumbani na kupatiwa chakula kutoka nyumbani.
Wanadai kuwa miongoni mwao wengine ni wagonjwa wa vidonda vya tumbo na hawawezi kula, kitendo ambacho kinakwenda kinyume na miiko ya kitabibu na kuzuiwa kuonana na familia zao.
Madai mengine ni kuzuiwa kuwaona kwa uhuru mawakili wao, wanafamilia kusikiliza kesi zao, masharti magumu na yasiyotekelezeka kama kuwataka washtakiwa wapate dhamana ya watu ambao wanafanya kazi serikalini,  mahabusu hao kutengwa kila mtu chumba chake.
Pia, wanafamilia hao wanadai kuwa watuhumiwa wananyimwa haki ya kuabudu kwa kunyimwa vitabu vya Qur’an na kuzuiwa kuswali pamoja wakati mahabusu wengine wanaruhusiwa.
“Huu ni udhalilishaji unaopita mipaka ya binadamu na kinyume na sheria za nchi yetu inayodai ni ya demokrasia, ni kinyume cha sheria za kimataifa ambazo Tanzania imezikubali,”  inadai sehemu ya barua hiyo.
Nakala za barua hiyo zimetumwa kwa Mwanasheria Mkuu Zanzibar, Kamishna Chuo cha Mfunzo Zanzibar, Waandishi wa Habari Tanzania, Waislamu wote Tanzania na Mkurugenzi wa Mshtaka Zanzibar (DPP).
Washtakiwa hao wapo rumande na kesi zao zinatarajiwa kuendelea tena Novemba 20, mwaka huu.

No comments:

Post a Comment