Sunday, November 18, 2012

DK. NCHIMBI AWAONYA WANAVYUO DODOMA

MKUU WA MKOA Dodoma, Dk. Rehema Nchimbi amewataka wanafunzi wa vyuo vya elimu ya juu walioko katika mkoa huo kujihoji nafsi zao na kucheki matendo yao kama kweli ni ya kumpendeza Mungu kwa vile ndiyo yanachangia wao kutotambua umuhimu wa nafasi walizonazo.

Dk. Nchimbi ametoa kauli hiyo mwishoni mwa wiki wakati akihutubia maelfu ya wanavyuo waliohudhuria Jumuiko la Wanavyuo wa Dodoma (Dodoma Campus Night) lililoambatana na mkesha wa kusifu na kuabudu uliofanyika kwenye ukumbi wa Chimwaga mjini Dodoma.

Jumuiko hilo lilihudhuriwa na wanafunzi zaidi ya 3,500 wa dini mbalimbali kutoka vyuo vikuu vya Dodoma (UDOM), St. John’s, Vyuo vya Mipango, Madini, Mirembe, Hombolo, Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE) na vyuo vya ualimu vya Mitumba na Capital.

Dk. Nchimbi alisema wanavyuo wengi ambao walifaulu kidato cha sita kwa alama za juu (first class) huwa wanaporomoka kimasomo wanapoingia kwenye vyuo vya elimu ya juu kwa sababu hawajiweki sawa kwenye mahusiano yao na Mungu aliyewaumba. “Wanaharibikiwa kwa sababu hawajiweki sawa na Mungu... hawakai pale ambapo Mungu anataka wawe (their right position),” alisema.

Alisema idadi kubwa ya wanavyuo wakishapata fedha za mkopo hutumbua maisha kwenye vilabu vya muziki ambavyo ni maarufu mjini humo kama vile Club 84, Club La Aziz na Maisha Club na hawarudi vyuoni hadi fedha yote imekwisha.

Alisema yeye kama mzazi analazimika kuyasema hayo kwa sababu anatambua kuwa watoto wa leo wamezungukwa na mitego mingi. “Hatutaki shetani awachezee, ndiyo maana tunawaonya,” alisisitiza.

Alisema katika kundi kubwa kama hilo wamo viongozi wa kesho na kwamba wasipojihadhari na kuweka mahusiano yao sawa na Mungu kuanzia sasa, watajikuta wanafanana na baadhi ya viongozi nchini ambao wamekabidhiwa dhamana lakini wanakengeuka na kufanya kinyume na matarajio ya wengi.

Mapema, akimkaribisha Mkuu wa Mkoa kuzungumza na wanafunzi hao, Mchungaji Gerald ole Nguyaine wa Kanisa la ICC –TAG Dodoma alisema wanafunzi walio katika vyuo hivyo ni wababa na wamama wa kesho hivyo hawana budi kumtanguliza Mungu katika yote wayafanyayo.

Naye Mchungaji Gavin Walker kutoka Kanisa la Calvary Christian Fellowship lililoko Columbus, Ohio, Marekani ambaye alikuwa mnenaji mkuu katika mkesha huo, aliwasihi wanavyuo kutambua makusudi ya Mungu ambayo ameyaweka juu yao. “Mungu amekuumba wewe kwa kusudi maalum hivyo ni lazima ujue hilo kusudi”, alisema.

Alisema kwa kutotambua kusudi la Mungu katika maisha yao, wako watu ambao wamejikuta wakitaka kufanana na wengine bila kujua ni kwa nini watu hao wamekuwa hivyo. “Wanatamani nafasi za wengine kwa sababu tu wao ni maarufu, ni waigizaji, ni wacheza sinema ama wasanii... hapana! Kila mmoja anatakiwa kujua kusudi ka Mungu katika maisha yake,” alisisitiza.

Irene K. Bwire,

No comments:

Post a Comment