Sunday, April 29, 2012

Ushindi wa mabao mengi utaisaidia Simba






WAWAKILISHI pekee wa Tanzania katika michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika, Simba leo inashuka dimbani jijini Dar es Salaam kucheza mchezo wa kwanza raundi ya tatu ya mashindano hayo dhidi ya timu ya  Al Ahly Shendi ya Sudan.
Simba ilifika hatua hiyo baada ya kutumia nguvu nyingi kuziondoa kwenye mashindano miongoni mwa timu bora na ngumu katika kinyang'anyiro hicho,  Kiyovu ya Rwanda na ES Setif ya Algeria.
Ilitoka sare ya bao 1-1 na wawakilishi wa Rwanda katika mchezo walioanza ugenini, na kisha kuja kushinda mabao 2-1 katika mchezo wa marudiano jijini Dar es Salaam.
Raundi ya pili, iliifunga ES Setif 2-0 kwenye mechi ya nyumbani, na kisha kufungwa mabao 3-1 ugenini, kipigo ambacho hakikuwazuia kusonga mbele kutokana na sheria ya faida ya bao la ugenini.
Kabla hata ya kutoa kauli yetu kwa wawakilisha hao, tunaamini wanaelewa umuhimu wa mchezo huo na hasa zaidi ukizingatia wanaanza nyumbani na kwenda kumaliza ugenini.
Tunafahamu wamejiandaa kupambana kufa na kupona lengo likiwa ni kupata ushindi mnono nyumbani ili kuepuka kujitwisha mzigo mzito wa kutafuta ushindi kwenye mchezo wa marudiano.
Tunasema hivyo kwa sababu, ushindi wa mabao mengi bila kuruhusu bao utawasaidia kuifanya mechi ya marudiano jijini Khartoum kuwa ya kukamilisha ratiba tu.
Tunapenda kuikumbusha Simba kutumia fursa hii ya kuanza nyumbani kuhakikisha wanapata ushindi mkubwa, na hilo linawezekana iwapo tu wachezaji watajituma muda wote wa mchezo.
Ikumbukwe,  Al Ahly Shendi siyo timu ya kubezwa pamoja na kwamba inashiriki michuano hiyo kwa mara ya kwanza, lakini iliweza kuiondoa kwenye mashindano Ferroviario Maputo kwa kuifunga bao 1-0 ugenini, na kisha wakashinda 2-0 kwenye mchezo wa marudiano nyumbani.
Tunatarajia Simba ambayo haisumbuliwi na wachezaji majeruhi itafanya vizuri katika mechi ya kesho kama inavyofanya vizuri katika mechi za Ligi Kuu ya Tanzania bara, ambapo inaongoza ligi hiyo.
Tunaitakia kila la kheri Simba.   SHUURANI KWA MWANACHI COMMUNICATION

No comments:

Post a Comment