Tuesday, July 30, 2013

JK FUNIKA KOMBE


RAIS Jakaya Kikwete ameshindwa kutanzua mgogoro wa ufisadi wa miradi ya maendeleo katika Halmashauri ya Manispaa ya Bukoba, badala yake amejielekeza kuwataka Meya Anatory Amani na Mbunge, Balozi Khamis Kagasheki, kumaliza tofauti zao.

Kauli yake imepingwa vikali na baadhi ya madiwani wakidai kuwa kiongozi huyo hafahamu kwa undani kiini cha mgogoro husika kuwa ni masilahi ya wananchi.

Juzi akihutubia mkutano katika Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba, Rais Kikwete alisema ujenzi wa soko kuu la kisasa katika manispaa hiyo lazima uendelee na kwamba hakuna hoja ya kuendelea na malumbano yasiyokuwa na msingi.
Alisema kuwa mbunge na meya wakiendelea kutiliana shaka wanaoumizwa ni wananchi, hivyo kuwaagiza viongozi hao kumaliza tofauti zao kwa kile alichodai hakuna lisilokuwa na mwisho.


Wakizungumza na gazeti hili jana kwa masharti ya kutotajwa majina yao, baadhi ya madiwani hao walieleza kushangazwa na kauli ya rais kuwa mgogoro huo ni jambo dogo.
Wakizungumza kwa hisia kali walisema kuwa hoja si ugomvi kati ya meya na Kagasheki bali hawakubaliani na jinsi meya huyo anavyotaka kuendesha miradi hiyo mitatu kifisadi.
Madiwani hao wa CCM walidai kuwa rais amepotoshwa kwa kuelezwa kwamba mgogoro huo ni baina ya Amani na Balozi Kagasheki wakati hoja hiyo iliasisiwa na madiwani wa CHADEMA kisha mbunge wao na madiwani wengine kuunga mkono.

“Shida yetu si kupinga miradi hiyo mitatu ya ujenzi wa soko la kisasa, kituo cha mabasi wala upimaji na ugawaji wa viwanja. Tatizo ni jinsi meya anavyotaka kuendesha miradi hiyo kifisadi bila kutushirikisha sisi kama wawakilishi wa wananchi.
“Wakati wenzetu wa CHADEMA wanaanza kupinga utekelezwaji wa miradi hii tuliwabeza na kudhani ni mambo ya kisiasa, lakini baadaye tukabaini kwamba meya anatuuza, hivyo baadhi yetu akiwamo Kagasheki tuliamua kuwaunga mkono,” walisema.
Madiwani hao walisisitiza kuwa mgogoro huo hauwezi kumalizwa kienyeji kiasi ambacho Rais Kikwete anataka bila meya Amani kuachia ngazi.
“Hapa Bukoba wananchi hawana imani tena na meya, huyu ana masilahi yake binafsi na anakumbatiwa na baadhi ya viongozi wa CCM na serikali wanaonufaika naye, hivyo msimamo wetu uko pale pale lazima ang’oke ndipo miradi iendelee,” alisema diwani mmoja.
Katika kuonesha kukasirishwa na msimamo wa rais, madiwani hao walisema kuwa leo watawasilisha barua yao kwa mkurugenzi wa manispaa ili kumtaka aitishe kikao cha kupiga kura ya kutokuwa na imani na meya.
“Rais anasema haya ni mambo madogo ambayo hayapaswi kufika kwake. Huyu ni kiongozi wa aina gani asiyefuatilia mgogoro huu wa dhuluma kwa wananchi wake? Hana taarifa kama CCM imepoteza wafuasi kwa sababu ya meya?” alihoji diwani mwingine.
Chimbuko la mgogoro
CHADEMA kupitia kwa viongozi wake wa Wilaya ya Bukoba Mjini wakiwamo madiwani wake wanne, ndio waliasisi hoja za kupinga miradi ya kifisadi iliyoingiwa na Amani pasipo kufuata utaratibu wa kisheria.
Kupitia uhamasishaji wa mikutano ya hadhara, viongozi hao waliwaelimisha wananchi kuhusu hasara itakayotokana na utekelezaji wa miradi hiyo, japo walipata upinzani mkubwa kutoka kwa meya na madiwani wa CCM.
Miradi hiyo ni upimaji wa viwanja 5,000 unaodaiwa mkopo wake wa sh bilioni 2.9 kutoka Mfuko wa Dhama ya Uwekezaji (UTT) haukufuata taratibu, na wananchi hawakushirikishwa ipasavyo.
Tuhuma nyingine ni mradi wa ujenzi wa soko. Meya anadaiwa kusitisha malipo ya ushuru na kutaka kuwaondoa wafanyabiashara bila kufuata utaratibu.
Anatuhumiwa pia kukopa sh milioni 200 kutoka Benki ya Uwekezaji (TIB) bila kibali cha Baraza la Madiwani. Vile vile alitoa taarifa kwenye kikao cha baraza hilo kuwa TIB iliwapa ruzuku ya sh milioni 90, lakini hakueleza misingi yake.
Upo pia mradi wa kuosha magari ambao unadaiwa kutumia kiasi cha sh milioni 297 zinazotiliwa shaka. Ameshindwa pia kutoa mchanganuo wa mapato na matumizi ya mradi wa kiasi cha sh milioni 134, za ujenzi wa kituo cha mabasi.
Awali, wakati CHADEMA wakitoa shutuma hizo dhidi ya meya, Mbunge wa Bukoba Mjini, Balozi Kagasheki na Meya Amani lao lilikuwa moja. Wote walitamba hadharani kwamba miradi hiyo lazima itekelezwe.
Hata hivyo, kuelekea mwishoni mwa mwaka jana, katika moja ya vikao vya Baraza la Madiwani, mbunge alishtuka baada ya kubaini kwamba hoja za CHADEMA zilikuwa za kweli, na kwamba miradi inayosimamiwa na meya itawaletea wakazi wa Bukoba maumivu ya muda mrefu mbele ya safari.
Alimpinga meya hadharani, hata akaitisha mkutano wa hadhara ambao ulihudhuriwa pia na Meya Amani; akasema yeye kama mbunge hawezi kukubaliana na meya katika miradi ya kifisadi.
Hatimaye, madiwani wengine wanane wa CCM wakaona hoja ya mbunge ina mantiki; na baada ya kutaka maelezo yenye mantiki wakayakosa, wakashawishi wenzao wa CUF kusaini azimio la kumwondoa meya.
Madiwani hao ni Alexander Ngalinda (Buhembe), ambaye pia ni naibu meya; Yusuf Ngaiza (Kashai) ambaye pia ni mwenyekiti wa CCM wa wilaya, Richard Gaspar (Miembeni), Deusdedit Mutakyahwa (Nyanga) na Robert Katunzi (Hamugembe).
Wengine ni Dauda Kalumuna (Ijuganyondo), Ibrahim Mabruk (Bilele), Rabia Badru na Murungi Kichwabuta wa Viti Maalumu.
Hata hivyo, baada ya Kagasheki kuibeba hoja ya CHADEMA akiungana na madiwani wengine wa CCM na CUF, alihitaji kuungwa mkono na madiwani wanne wa CHADEMA ili kukamilisha akidi inayoweza kupiga kura ya kumwondoa meya.
Kwa kugundua hilo, meya naye anadaiwa kuingilia ngome ya CHADEMA ili kuwagawa na kupunguza kura.
Baada ya muda mfupi, wakati shinikizo la kumwondoa meya likiwa limepamba moto, uongozi wa CHADEMA manispaa ulikaa na wabunge wake katika kikao ambacho kiliisha kwa mgawanyiko.
Madiwani wawili wa CHADEMA, Dismas Rutagwelera (Rwamishenyi) na Israel Mulaki (Kibeta), waliingia kikaoni wakiwa na msimamo wa kukataa katakata kupiga kura ya kumwondoa meya, kwa kigezo kuwa hiyo hoja si yao bali ya CCM.
Kwa sababu hiyo, madiwani wawili waliobaki, Conchesta Rwamlaza na Winfrida Mukono, waliendelea kushikilia msimamo wa awali, kwamba meya aondoke.
Kundi la Rwamlaza na Mukono linaamini kwamba wao ndio waasisi wa hoja ya ufisadi wa meya, na kwamba wangekuwa watu wa ajabu kuachana nayo eti kwa vile imeungwa mkono na madiwani wa CCM.
Wakati hali ikiwa hivyo CHADEMA, uamuzi huo wa madiwani uliigawa pia CCM na kuonekana kama ugomvi kati ya Kagasheki na Amani. Kutokana na mpasuko kuwa mkali CCM taifa ililazimika kuingilia kati.
Makamu Mwenyekiti wa CCM taifa, Philip Mangula, alifika Bukoba Februari mwaka huu na kukutana na uongozi wa CCM wilaya wakiwamo madiwani na kuwaagiza waondoe tuhuma zao dhidi ya meya, akidai walikiuka utaratibu.
Hatua hiyo ilizidi kukuza mgogoro, hivyo Katibu wa Itikadi na Uenezi taifa, Nape Nnauye, kulazimika kuingilia kati kwa kuiomba Wizara ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa kuunda tume ya kuchunguza tuhuma hizo.
Tume hiyo iliundwa na kwenda Bukoba kuchunguza tuhuma hizo ingawa hadi Rais Kikwete anawataka meya na mbunge wamalize tofauti zao ripoti bado haijatolewa.
Rais Kikwete aliagiza kuwa kabla ujenzi huo wa soko haujaanza wahakikishe wananchi wanapatiwa  eneo mbadala ambalo litakuwa la muda kwa ajili ya kuendelea  na shughuli zao za biashara wakati wakisubiri  kukamilika kwa ujenzi.
Alisema wafanyabiashara wa soko hilo  wasiharibiwe maisha yao, hata kama wapo kwenye soko la zamani bado wapate riziki zao katika soko hilo.
Kwamba, baada ya kukamilika kwa ujenzi wa soko hilo, wafanyabiashara waliokuwepo awali ndio wapewe kipaumbele katika soko jipya.
Pia aliagiza Halmashauri ya Manispaa ya Bukoba kuwagawia  viwanja 800 wananchi waliokuwa wamelipa fedha kwa ajili ya kupimiwa viwanja mwaka 2003 kwa sh 50,000 hadi sh 70,000 kutoka katika mradi wa viwanja 5,000 wa sasa bila kuwatoza nyongeza ya fedha ya ziada.
Alihoji ni kwa nini wananchi hao hawakupewa viwanja wakati wamelipa na hata baada ya kukosa viwanja ilikuwaje wasirudishiwe fedha zao.
Aliwata halmashauri kujihesabu kuwa wao ndio waliochelewa kuwapa wananchi viwanja hivyo, kwamba wawapatie sasa, fidia watajua wenyewe jinsi ya kufidia kiasi cha fedha kinachohitajika.

No comments:

Post a Comment