WATOTO wa shule, wafanyabiashara na watalii kutoka
duniani kote, ikiwa ni pamoja na Wajerumani, wanamiminika kwenye nyumba
ya zamani ya mzee Nelson Mandela katika kitongoji cha Soweto kumtakia
afya njema.
Hali ya Mandela yasemekana imekuwa nzuri kidogo japokuwa
bado yu chumba cha wagonjwa mahututi.
Wakati Mandela mwenyewe amelazwa hospitalini bado akiwa katika hali
mbaya, watoto wa shule wa Afrika Kusini, hapo jana walijipanga katika
foleni ndefu mbele ya nyumba ambamo Mandela aliishi hapo zamani katika
kitongoji cha waafrika cha Soweto kilichopo Johannesburg.
Mtoto mmoja ameeleza sababu ya kwenda kuitembelea nyumba hiyo
akisema, “Yeye ni kama baba yangu. Nampenda Mandela. Nampenda sana.”
Mwalimu wa watoto hao amesema wakati Mandela amelazwa hospitalini
wameamua kwenda kwenye nyumba ya zamani ya Mandela, licha ya kuwa na
mapumziko. Mwalimu huyo amesema watoto hao wenye umri kati ya miaka
minane na kumi wanajifunza mengi juu ya Mandela shuleni. Lakini jee
wanajua nini hasa juu yake.
Mtoto mmoja amesema, “Yeye ndiye aliyetukomboa. Tumekuja hapa ili
kumwonyesha jinsi tunavyompenda.” Mtoto mwengine amesema, “Kwangu mimi
Mandela ni shujaa kwa sababu aliupigania uhuru wetu.”
Watu kutoka sehemu mbalimbali za dunia, ikiwa pamoja na watalii wa
kijerumani pia wanakendwa katika nyumba ya zamani ya Nelson Mandela.
Msimamizi wa nyumba hiyo ambayo sasa imekuwa ya makumbuisho, Jane
Monakwane, amesema idadi ya watu wanaoenda katika nyumba hiyo ya
ukumbusho sasa imeongezeka. Patashika kubwa ya kuitembelea nyumba hiyo
inaweza kufafanishwa na tukio la mwaka wa 1990 katika historia ya Afrika
ya Kusini wakati ambapo Mandela, aliyekuwa mfungwa maarufu duniani
alifunguliwa na kurejea katika maskani yake ya Soweto. Hata hivyo
hakuendelea kukaa hapo kwa muda mrefu.
Mkuu wa makumbusho, Jane Monakwane, ameeleza kwa nini Mandela hakukaa
katika nyumba hiyo kwa muda mrefu. “Nafikiri baada ya kuwamo kifungoni
kwa miaka 27, Mandela hakutambua jinsi alivyogeuka kuwa mtu maarufu
sana.” Mandela alikaa katika nyumba yake ya Soweto kwa muda wa siku 11
pamoja na mkewe wa hapo zamani Winnie. Lakini kutokana na kusongwa na
waandishi wa habari na watu wengine Mandela alihamia katika kitongoji
cha watu wenye hali nzuri cha Houghton.
Watoto wa shule, wafanyabiashara na watalii wanaoitembelea nyumba ya
Mandela ya Soweto pia wanaifuatilia hali yake wakati akiwa amelazwa
hospitalini. Mtalii mmoja kutoka Ujerumani, Gisela Seemann, amesema
ikiwa Mandela ni mgonjwa sana kiasi cha kusibika basi ni vyema
lipatikane suluhisho. Lakini karibu na nyumba hiyo ya makumbusho pana
bango la nembo ya kinywaji cha Whiskey; Johnny Walker, Yohana Mtembezi,
likiwa na maana ya kumtakia Madiba uwezo wa kuendelea kutembea hadi
afikie umri wa miaka 95.
-DW
No comments:
Post a Comment