Tuesday, March 12, 2013

MAMA AUAWA KWA MAPANGA MBELE YA WATOTO WAKE


Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Ernest Mangu
Ikiwa ni siku chache tu tangu dunia ilipoadhimisha Siku ya Wanawake Machi 8 mwaka huu, mauaji ya wanawake yameendelea kushika kasi nchini, ambapo katika kitongoji cha Senta  A, katika kijiji cha Bupandwa, wilayani sengerema, mkoani Mwanza mwanamke mmoja ameuawa kikatili kwa kukatwa mapanga kisha mkono wake kuondolewa baada ya kuvamiwa nyumbani kwake na watu
wasiojulikana.
 
Aliyeuawa ametambulika kwa jina la Juliana Masele (55) mkazi wa kijiji hicho ambaye alivamiwa nyumbani kwake majira ya saa 2:30 usiku wa kuamkia jana na watu wasiojulikana wakati akila chakula cha usiku na watoto wake wanne.
 
Baada ya watu hao kumvamia walimkata kwa mapanga sehemu mbalimbali za kichwa kisha kuukata mkono wake wa kushoto hadi kudondoka chini hali iliyosababisha kutokwa na damu nyingi zilizopelekea mauti yake.
 
Akizungumza na NIPASHE, mmoja wa watoto wa mama huyo ambaye alishuhudia tukio hilo, Masele Japhet, lilitokea wakati mama yake akila chakula cha usiku na watoto wake ambapo watu
wasiofahamika waliwavamia na kufanya mashambulizi hayo kwa
kutumia mapanga huku wakiwa wamevalia makoti marefu na kufunika nyuso zao mithili ya ninja.
 
Alisema baada ya kumjeruhi mama yao watu hao waliondoka pasipo kuchukua kitu chochote wala kumdhuru mtu mwingine na kwamba hakuna taarifa zozote walizoziacha hivyo hawajafahamu chanzo cha watu hao kuamua kufanya mauaji ya mzazi wao.
 
Mwenyekiti wa kijiji hicho, Vicent Thobias, alisema unyama huo ulifanywa na watu wawili waliokuwa na silaha za jadi ambao baada ya kutekeleza mauaji hayo walitoweka na kutelekeza panga moja lililotumika kwenye mauaji hayo.
 
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Ernest Mangu amethibitisha kutokea kwa mauaji hayo na kwamba jeshi lake linaendelea na upelelezi ili kubaini waliohusika na unyama huo ili waweze kufikishwa mahakamani

No comments:

Post a Comment