Saturday, November 7, 2015

MAGUFULI AANZA KAZI ASITISHA SAFARI ZA NJE NCHI KWA WATENDAJI WAKUU


 
Umbali wa takribani kilomita moja kutoka ofisini kwake Ikulu jijini Dar es Salaam, Rais Dk.John Magufuli anatembea hadi Wizara ya Fedha anapowakuta ‘wazembe’ wakiwa nje ya ofisi.
 
Tukio hilo la jana lilikuwa la kushtukiza, lisilotarajiwa na wakazi wa jijini kumuona Rais Magufuli akiwa katika siku ya pili ya utawala wake, ‘akikatiza’ kwa mguu kwenda wizarani hapo.
 
Akiwa katika kampeni na baada ya kutangazwa mshindi wa kiti cha urais, Rais Magufuli aliwaonya watumishi wa umma kuacha kufanya kazi kwa mazoea na uzembe na wasioweza mabadiliko, waanze kuondoka.
 
Akiwa katika kuthibitisha kauli mbiu yake ya ‘hapa ni kazi tu’, Rais Magufuli aliingia wizarani hapo na kukuta baadhi ya viti sita vikiwa wazi, taarifa ikaeleza kwamba watumishi wahusika walikuwa nje ya ofisi kunywa chai.
 
Ili kupata ushahidi usiotiliwa shaka, Rais Magufuli alishika kiti kimoja baada ya kingine, akiuliza jina la mtumishi anayekitumia na mahali alipo.
 
Ziara hiyo aliifanywa muda mfupi baada ya kumuapisha Mwanasheria Mkuu wa Serikali, George Masaju aliyemteua katika siku ya kwanza ya utawala wake.
 
Tukio hilo ambalo lilikuwa ni la aina yake liliwashangaza baadhi ya wananchi na kujikuta wakimshangilia kila alipopita.
Alipofika katika wizara hiyo alianza kuingia ofisi moja baada ya nyingine huku akihoji baadhi ya wafanyakazi ambao hawakuwepo wakati huo wa kazi.
 
“Hiki kiti ni cha nani, amekwenda wapi… na nayekalia kiti kile yule anaitwa nani… ina maana hawa wote sita hawapo  wameenda wapi wakati wewe ni bosi  wao au wameenda kunywa chai… haya ,” alihoji Rais Magufuli.
 
Aliwata watendaji wakuu wa wizara hiyo kutekeleza majukumu yao kikamilifu kwa kukusanya kodi hasa kutoka kwa wafanyabiashara wakubwa ambao wanadaiwa kuikwepa.
 
Alitoa rai kama hiyo kwa Mamlaka ya Kodi (TRA) akitaka watii na kufuata sheria katika utendaji kazi wao.
Rais Magufuli alisema katika serikali yake hakuna kiongozi yeyote serikalini atakayetoa ‘memo’ kwa TRA kusamehe ulipaji wa kodi  halali za serikali.
 
Alisema kodi inaiwezesha serikali kutoa huduma za kijamii kama elimu ya bure kuanzia kidato cha kwanza hadi cha nne kuanzia mwakani.
 
Aidha, aliagiza kampuni zinazotangaza kufilisika kutoa taarifa sahihi serikalini kuhusu ulipaji kodi za serikali ulivyofanywa na mhusika.
 
POSHO KWA WABUNGE
Rais Magufuli alipiga marufu malipo ya posho kwa wabunge yanayofanywa nje ya zile wanazolipwa na Bunge.
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment