Friday, September 4, 2015

MAGUFURI AWAHAKIKISHIA WAANDISI WAZAWA

Mgombea urais kupitia tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk John Magufuli akiendesha mtambo maalumu unaochanganya saruji, kokoto na udongo katika ujenzi wa barabara ya Tunduru-Mangaka, eneo la Kilimasera-Matemanga la kilometa 68.2 juzi. (Na Mpigapicha Wetu).


WAZIRI wa Ujenzi, Dk John Magufuli amewahakikisha wahandisi kwamba endapo atachaguliwa kuwa Rais wa serikali ya Awamu ya Tano hatawaangusha na atahakikisha anawatumia vyema kwa ajili ya kujenga uchumi kutoka wa chini kwenda wa kati.
Dk Magufuli ambaye pia ni mgombea urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) aliyasema hayo jana Dar es Salaam wakati akifunga maadhimisho ya Siku ya Wahandisi Tanzania 2015 yaliyowashirikisha wahandisi kutoka ndani na nje ya nchi.
“Nawahakikishia wahandisi Mungu akijaalia kule mbele siwezi kuwaangusha, siku za nyuma nilikuwa naagizwa ila sasa nitakuwa naagiza mimi, hivyo msiwe na wasiwasi na maamuzi nitakayoagiza na kufanya yatakuwa kwa faida ya wahandisi na Watanzania wote,” alisema.

Alisema amekuwa serikalini miaka 15 na amekuwa wizara ya ujenzi na katika miaka hiyo maisha yake yamekuwa na uhusiano mkubwa na wahandisi na amejifunza mengi kupitia wao na ni sekta ambayo anatambua manufaa yake na changamoto zake, hivyo hataweza kuwaacha.
“Duniani popote sehemu iliyofanikiwa ni sehemu ambayo palikuwa na wahandisi na wametumiwa vizuri, hivyo nami nitahakikisha nawatumia sana katika kujenga uchumi na tunataka kuhakikisha sekta ya maji na viwanda inakuwa,” alisema.
Aidha alisema endapo akichaguliwa ataanzisha mamlaka katika halmashauri itakayohusu masuala ya wahandisi kama ilivyo Tanroads ili kuwawezesha kupata bajeti yao watakayoisimamia wenyewe bila kuingiliwa na wanasiasa.
Aliongeza kuwa, “pamoja na kwamba sijaja kuwaomba kura ila ni vyema mkamchagua mtu anayewafahamu wahandisi vizuri maana hatawaangusha… lakini naomba niwaombe kura msije mkasema sikuwaomba, naombeni kura zenu”.
Aliwakemea baadhi ya wahandisi ambao wamekuwa wakiharibu sifa ya wahandisi kwa kufanya kazi chini ya kiwango na kuwataka kubadilika na kufanya kazi kwa weledi ili kuendelea kujenga sifa nzuri na kupata kazi nyingi zaidi.
Mapema Naibu Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Joseph Nyamuhanga alisema tangu mwaka 2005-2015 ujenzi wa barabara umeimarika ambapo barabara nyingi zimejengwa na zingine zipo katika hatua mbalimbali.
Alisema katika kipindi hicho wamejenga madaraja makubwa 12 na yamekamilika pamoja na madogo 7,200 na mengine saba yanaendelea kujengwa likiwemo la Kigamboni na Kilombero.
Mwenyekiti wa Bodi ya Usajili wa Wahandisi, Profesa Ninatubu Lema alisema wamejipanga kuendelea kulitumikia taifa ili ifikapo 2025 waweze kujivunia kulitoa taifa kutoka uchumi wa chini kwenda wa kati.

No comments:

Post a Comment