Thursday, May 21, 2015

CCM NGOMA NZITO DODOMA

 
 Mwenyekiti wa chama cha mapinduzi CCM

Mambo yanaonekana kuwa mazito kwa CCM ambayo inajiandaa kufanya moja ya mikutano yake muhimu ya vyombo vyake vya juu kabla ya kuanza mchakato wa Uchaguzi Mkuu baada ya Sekretarieti kukutana hadi usiku wa manane kufanya maandalizi ya vikao hivyo.
Vyombo hivyo vya juu vya CCM, Kamati Kuu na Halmashauri Kuu vitakutana kuanzia kesho kupanga utaratibu wa mchakato wa Uchaguzi Mkuu, huku vikitakiwa kufanya maamuzi mazito kuhusu makada wanaotaka kuwania urais ambao wamefungiwa pamoja na mawakala ambao wamekuwa wakiendesha kampeni za kutaka wagombea hao waungwe mkono.
Sekretarieti ya chama hicho ilikutana kuanzia juzi hadi usiku wa manane kufanya maandalizi na jana kufuatiwa na Kamati ya Kanuni ambayo inatazama upya kanuni za uchaguzi za chama hicho ambazo zinaweza kuwagusa wagombea wanaoonekana kukiuka taratibu.
Vikao hivyo vinafanya kazi ya kuandaa na kuthibitisha ajenda za vikao vikuu huku ajenda muhimu katika mikutano hiyo ikiwa ni hali ya kisiasa nchini, maandalizi ya uchaguzi mkuu, mchakato wa namna ya kuwapata wagombea wa CCM wa ngazi zote na ratiba ya uchaguzi.
Vikao hivyo pia vitapewa taarifa ya maandalizi ya ilani ya chama na kutoa maoni.

 
Habari zilizolifikia gazeti hili jana zilisema kuwa kikao cha sekretarieti ya chama hicho inayoongozwa na Katibu Mkuu Abdulrahman Kinana kiliketi juzi kuanzia 10:00 jioni hadi sasa 6:00 usiku, lakini hakikumaliza kazi yake, hivyo kitaendelea leo.
“Jana (juzi) walikaa hadi sasa 6:00 usiku na leo (jana) wamepumzika, lakini kesho (leo) wataendelea tena na vikao vya Sekretarieti,” alisema mmoja wa maofisa wa chama hicho ambaye hakutaka kutajwa jina lake kwa kuwa si msemaji.
Habari zaidi kutoka ndani ya ofisi za makao makuu ya CCM, maarufu kama White House zinasema kuwa wajumbe wa Kamati ya Kanuni walikutana jana jioni kuangalia upya kanuni za uchaguzi.
Hata hivyo, chanzo kingine cha habari kilieleleza kuwa huenda kamati hiyo ya kanuni ndiyo ile ile inayoandaa ilani ya uchaguzi ya CCM 2015-2020 inayoongozwa na Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Stephen Wasira, ambaye pia anatajwa kuwania urais.
Wakati wajumbe hao wakiendelea na vikao ndani ya ofisi hiyo ya makao makuu, magari ya viongozi wa Serikali ambao ni wajumbe yalionekana nje yakiwamo ya mawaziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika (Wasira), Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi na Waziri wa Nchi katika Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano, Samia Suluhu Hassan.
Wakati vikao hivyo vikiendelea wajumbe, wengine wa Halmashauri Kuu, Kamati Kuu na maofisa wa chama walitarajiwa kuanza kuingia mjini hapa jana jioni kutoka maeneo mbalimbali, huku wapambe wa wagombea urais wakiwa wameshaanza kuingia.
Kikao cha Halmashauri Kuu ya Kamati Kuu ya CCM, kinatarajiwa kufanyika kesho, kikifuatiwa na kikao cha Halmashauri Kuu kitakachokaa kwa siku mbili.

No comments:

Post a Comment