
Mwenyekiti wa chama cha mapinduzi CCM
Mambo yanaonekana kuwa mazito kwa CCM ambayo inajiandaa kufanya
moja ya mikutano yake muhimu ya vyombo vyake vya juu kabla ya kuanza
mchakato wa Uchaguzi Mkuu baada ya Sekretarieti kukutana hadi usiku wa
manane kufanya maandalizi ya vikao hivyo.
Vyombo hivyo vya juu vya CCM, Kamati Kuu na
Halmashauri Kuu vitakutana kuanzia kesho kupanga utaratibu wa mchakato
wa Uchaguzi Mkuu, huku vikitakiwa kufanya maamuzi mazito kuhusu makada
wanaotaka kuwania urais ambao wamefungiwa pamoja na mawakala ambao
wamekuwa wakiendesha kampeni za kutaka wagombea hao waungwe mkono.
Sekretarieti ya chama hicho ilikutana kuanzia juzi
hadi usiku wa manane kufanya maandalizi na jana kufuatiwa na Kamati ya
Kanuni ambayo inatazama upya kanuni za uchaguzi za chama hicho ambazo
zinaweza kuwagusa wagombea wanaoonekana kukiuka taratibu.
Vikao hivyo vinafanya kazi ya kuandaa na
kuthibitisha ajenda za vikao vikuu huku ajenda muhimu katika mikutano
hiyo ikiwa ni hali ya kisiasa nchini, maandalizi ya uchaguzi mkuu,
mchakato wa namna ya kuwapata wagombea wa CCM wa ngazi zote na ratiba ya
uchaguzi.
Habari zilizolifikia gazeti hili jana zilisema
kuwa kikao cha sekretarieti ya chama hicho inayoongozwa na Katibu Mkuu
Abdulrahman Kinana kiliketi juzi kuanzia 10:00 jioni hadi sasa 6:00
usiku, lakini hakikumaliza kazi yake, hivyo kitaendelea leo.
“Jana (juzi) walikaa hadi sasa 6:00 usiku na leo
(jana) wamepumzika, lakini kesho (leo) wataendelea tena na vikao vya
Sekretarieti,” alisema mmoja wa maofisa wa chama hicho ambaye hakutaka
kutajwa jina lake kwa kuwa si msemaji.
Habari zaidi kutoka ndani ya ofisi za makao makuu
ya CCM, maarufu kama White House zinasema kuwa wajumbe wa Kamati ya
Kanuni walikutana jana jioni kuangalia upya kanuni za uchaguzi.
Hata hivyo, chanzo kingine cha habari kilieleleza
kuwa huenda kamati hiyo ya kanuni ndiyo ile ile inayoandaa ilani ya
uchaguzi ya CCM 2015-2020 inayoongozwa na Waziri wa Kilimo, Chakula na
Ushirika, Stephen Wasira, ambaye pia anatajwa kuwania urais.
Wakati wajumbe hao wakiendelea na vikao ndani ya
ofisi hiyo ya makao makuu, magari ya viongozi wa Serikali ambao ni
wajumbe yalionekana nje yakiwamo ya mawaziri wa Kilimo, Chakula na
Ushirika (Wasira), Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi,
William Lukuvi na Waziri wa Nchi katika Ofisi ya Makamu wa Rais,
Muungano, Samia Suluhu Hassan.
Wakati vikao hivyo vikiendelea wajumbe, wengine wa
Halmashauri Kuu, Kamati Kuu na maofisa wa chama walitarajiwa kuanza
kuingia mjini hapa jana jioni kutoka maeneo mbalimbali, huku wapambe wa
wagombea urais wakiwa wameshaanza kuingia.
Kikao cha Halmashauri Kuu ya Kamati Kuu ya CCM,
kinatarajiwa kufanyika kesho, kikifuatiwa na kikao cha Halmashauri Kuu
kitakachokaa kwa siku mbili.
No comments:
Post a Comment